Jumamosi, 9 Juni 2018

Mfupa wa Tukuyu Stars unavyotesa VPL

Gharib MZINGA
Abdul Lausi na Joseph Ksyupa ni miongoni mwa majina ambayo yameacha historia kubwa katika soka la Mkoa wa Mbeya, vijana hawa wawili ndio waliotoa wazo la kuunganisha vilabu viwili vya wilayani Rungwe Tukuyu Mkoani Mbeya, Mwenge FC na Jamuhuri FC mwanzoni mwa miaka ya 1980.
Dhumuni kubwa likiwa ni kunyanyua soka la Wilaya hiyo ili kupata timu itakayowakilisha katika ligi daraja la kwanza  (ligi kuu sasa).
Jitihada za Wanatukuyu wakiunganishwa na timu hiyo zilizaa matunda kwa kumpata mdhamini mkuu mfanya biashara Ramnik Patel Kaka.
Timu hiyo ya Tukuyu Stars ‘Banyambala’ ilianza harakati miaka ya 1982, ilifanikiwa kucheza michezo mingi ya kirafiki ya kimataifa ikiwa ligi daraja la 3 na 2, Ilicheza na timu ya taifa ya Msumbiji pia katika harakati za kujipanga katika kupigana kupanda ligi daraja la kwanza (ligi kuu sasa).
Mwaka 1985 Tukuyu Stars ‘Banyambala’ ilifanikiwa kupanda daraja na kuingia ligi daraja la kwanza rasmi, kikosi cha Tukuyu kiliundwa na wachezaji nguli kama vile Asanga Aswile, Mbwana Makata, Betwel Afrika, Daniel Chundu, Chachala Muya, Kelvin Haule, Peter Mwakibibi  na wengine.
Mwaka ho 1986 Tukuyu Stars ilifanikiwa kucheza ligi kuu na kubeba taji la ligi hiyo kipindi hicho ikidhaminiwa na kampuni ya bia ya Safari Lager.
Hii ni kumbukumbu kubwa katika historia ya soka la Tanzania na Africa kwa ujumla wakivilaza njaa vilabu vikongwe Simba na Yanga.
Baada ya mwaka huo miaka miwili mbele (1988) Tukuyu Stars ilishuka daraja na kuenda kusikojulikana, ilisababishwa na wachezaji wake wengi muhimu kuchukuliwa na vilabu vikongwe Simba na Yanga.
Baada ya Tukuyu Stars kuonesha uwezo na uthubutu hakuna timu nyingine iliyowahi kufanya ivyo.
Timu nyingi zimekua zikipanda na kushuka nyingine zikipanda na kubaki katika ligi huku zikiwa zinasuasua kubakia, Mbeya City msimu wake wa kwanza ilijaribu kuutafuna mfupa huo lakini ikashindwa, macho mengi yalielekezwa kwa Singida United huwenda ingethubutu lakini imeshindwa.
Timu nyingi ukiacha Simba na Yanga zimechukua taji la ligi  tangu ikiitwa daraja la kwanza mpaka sasa ligi kuu(VPL) Cosmopolitan 1967, Mseto 1974, Pan Africa 1982, Coastal Union 1988, Mtibwa  Sugar 1999/2000 na Azam FC 2013, lakini Tukuyu tu ndiyo iliyochukua taji hilo kwa msimu wake wa kwanza.
Nani ataweza kuutafuna mfupa wa Tukuyu Stars ‘Banyambala?  KMC, African Lyon, Biashara, Alliance, JKT Tanzania au Coastal Union?

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni