
AJALI ya bodabda imemuondoa kikosini beki wa Simba, Salim Mbonde baada ya kuondolewa katika kikosi kinachosafiri nchini kesho kuelekea nchini Misri kwa ajili ya mchezo wa marudiano dhidi ya Al Masry, Kombe la Shrikisho Afrika.
Simba itakuwa ugenini dhidi ya Al Masry katika mchezo huo wa marudiano utakaochezwa Jumamosi Uwanja wa Port Said mjini Port Said, Misri ikihitaji ushindi wowote kusonga mbele, baada ya sare ya 2-2 kwenye mchezo wa kwanza Dar es Salaam Jumatano wiki iliyopita.
Beki huyo alikuwa miongoni mwa wachezaji walikuwepo katika mipango ya Kocha Mkuu, Mfaransa Pierre Lechantre kumtumia katika mchezo huo kutokana na ajali hiyo iliyosababisha ashonwe nyuzi tatu juu kidogo ya jicho, amemuondoa katika mipango hiyo.
Mbonde alisema hatakuwepo katika mchezo huo kutokana na majeraha aliyopata katika ajari hiyo kwa kusababisha kushindwa kuendelea na mazoezi ndani ya kikosi cha Wekundu wa Msimbazi hao.
“Sitakuwepo katika msafara huo, suala la kuanza lini mazoezi bado sijajua kwani bado sijatoa nyuzi nadhani baada ya kurejea nitaungana na wenzangu baada ya kupata taarifa kutoka kwa daktari wa timu,” alisema Mbonde.
Beki huyo wa kati, amekutana na majanga hayo baada ya kutoka katika majeruhi yaliyomuweka nje tangu Oktoba 15 mwaka jana alipoumia kwenye mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara dhidi ya timu yake ya zamani, Mtibwa Sugar.
Kwa ujumla, Simba inawakosa mabeki wake wa kati waliounda ukuta imara mwanzoni mwa msimu, baada ya dirisha dogo pia kumuacha aliyekuwa Nahodha wake, Mzimbabwe, Method Mwanjali aliyekuwa anacheza pamoja na Mbonde.
Kwa sasa safu ya ulinzi ya Simba iliyopwaya inaundwa na chipukizi Yussuph Mlipili akishirikiana na ama na Erasto Nyoni, James Kotei au Juuko Murshid wakati mwingine – haina watu maalum bado.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni