Jumanne, 2 Januari 2018

TUIKUMBUKE TABORA JAZZ






TABORA JAZZ   ‘Wana Segere Matata’ ni bendi pekee ya muziki wa dansi  inayojulikana huko Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.
Kauli hiyo nzito ilitolewa na mkongwe wa muziki wa dansi toka Jamhuri  na Kidemokrasia ya Congo, Tabu Ley  Rochereau.

Akiwa ziarani hapa Tanzania, Tabu Ley aliwahi kufanya mkutano na waandishi wa habari katika hoteli Kilimanjaro. Moja kati ya  maswali aliyoulizwa ni kutaka kufahamu ni bendi gani hapa Tanzania wanayoijua huko kwao DRC. Tabu Ley pasipo kupepesa macho, alikiri kwa kujibu kwamba  ni Tabora Jazz pekee ndiyo inayojulikana huko.

Tabora Jazz ni bendi kongwe iliyoanzishwa mwaka 1954, ambao katika historia ya Tanzania ndiyo mwaka ambao chama cha TANU kilianzishwa.

Bendi hiyo ilikuwa  ikiongozwa na waanzilishi akina  Hamis Ali Songo na Mlekwa Selemani, ikiwa na makazi yake mjini Tabora ikipiga na kutoa burudani murua za muziki wa dansi katika kumbi za  Lumumba kwenye kona ya mitaa ya Usagara na Rufita ambako ndiko yalikuwa makao makuu yake. Pia walikuwa wakipiga katika Baa za Bizeta, Maua na nje ya mji wakialikwa.

Miaka ya nyuma Tabora Jazz ilikuwa na upinzani mkubwa na bendi ya Western Jazz ya jijini Dar es Salaam. Upinzani huo ulijiri baada ya Bendi ya Western Jazz kukwapua kwa nyakati tofauti nguli wawili toka Tabora Jazz., kwa ambao walihamisha ‘melody’ yao kuipeleka huko.

Wanamuziki hao walikuwa  akina Wema Abdallah na Rashidi Hanzuruni ambao walikuwa mahiri kwa kulicharaza gitaa la solo,ambao walihamisha ‘melody’ kuzipeleka Western Jazz.


Nyimbo nyingi za bendi hiyo zilipigwa mno katika  kituo cha Redio Tanzania Dar es Salaam (RTD) na kusikika  sehemu kubwa Afrika ya Mashariki na Kati.

Huko nchini Rwanda kulikuwepo redio Rwanda iliyokuwa na kipindi cha muziki nyakati za jioni kikiendeshwa na mtangazaji Kabendera Shinani, ambaye alikuwa akizipiga nyimbo za Tabora Jazz kila mara. Redio hiyo ilikuwa ikisikika hapa nchini maeneo mbalimbali ya mikoa ya Kigoma, Tabora, Shinyanga, Mwanza na Kagera (Ziwa Magharibi) wakati huo.

‘Wana Segere matata’ waliwika sana miongoni mwa bendi kubwa hapa nchini zikiwemo Morogoro Jazz, Cuban Marimba, Western Jazz, NUTA Jazz, Dar. Jazz, Kilwa Jazz, Urafiki Jazz, Jamhuri Jazz na nyingine nyingi.

Mji wa Tabora wakati huo ulikuwa na ushindani mkubwa katika muziki kati ya Tabora Jazz na bendi zingine zilizokuwepo wakati huo za Kiko Kids iliyokuwa ikiongozwa na Salimu Zahoro na Nyanyembe Jazz iliyoibuka na kibao chake cha ‘Rangi ya Chungwa’ wimbo ambao hadi sasa bado unarindima kwenye vituo vingi vya redio na kumbi nyingi  za burudani hapa nchini.
Pia mji wa Tabora enzi hizo kulikuwa na umkumbi mkubwa wa Disco uliokuwa ukijulikana kwa jina la ‘Mwana Isungu’ uliokuwa ikiteka kundi kubwa la  vijana wa mji huo kwa kuporomosha muziki maridhawa, zikiwemo nyimbo za Tabora Jazz na Nyanyembe Jazz.

Kama nilivyokudokeza hapo awali kwamba bendi hiyo ilianzaishwa kabla ya  Tanganyika kupata Uhuru, hivyo iliendeleza mfumo wa kikoloni. Mfano mmoja ni kwamba katika miaka ya 1960 ilikuwa ni marufuku kwa mpenzi au shabiki kuingia ukumbini kucheza muziki pasipo ‘kunyonga’ Tai shingoni, licha ya pesa zake. Hii ilikuwa ni moja ya njia ya kuzingatia utanashati na nidhamu  kwa ujumla.

Bendi hiyo ilipiga katika mitindo ya  Segere matata, Segua Segua, na Mambo Milekana, ikiwazingua wapenzi wa muziki mjini humo.
Miaka hiyo Tabora Jazz alitoka na nyimbo zao ngingi zikiwemo za Usijifanye mwewe, Mariam mpenzi, Zabibu No.2, Anna, Regina, Mambo Mileka, Tucheza Segere, Dada Mwantumu, Serafina,Tamaa yako, Alhamdulilah, Nashukuru sana, na Dada Asha.

Zingine ni pamoja na Zabibu, Halima, Dada Helena, Lucie, Farida na Dada Mwantumu.
Kufuatia ushindani mkubwa uliokuwepo mjini humo  kati yake na Nyanyembe Jazz na Kiko Kids, Tabora Jazz ilifumua vibao ingine vikali  vya Chakula kwa Jirani, Mapenzi hayana mganga, Mambo Mileka, Ujana una mwisho. Salima, Dada Remmy, Tucheze Segere na  Rukia wajidanganya.

‘Segere matata’ wakati huo ilikuwa na mashabiki waliokubuhu. Kwa wakazi wa Tabora mjini hawawezi kumsahau shabiki mmoja aliyejulikana kwa jina la ‘Mzee Segua’ ambaye alikuwa hakosi onyesho lolote la bendi hiyo akicheza ‘Segua Segua, mtindo aliokuwa aikiumudu hadi kufikia kupachikwa jina la ‘Mzee Segua’

Alikuwa ni Mzee mwenye vituko ukumbini, akiwa na mfanyakazi katika Ofisi moja ya serikali mjini humo  kama dereva. ‘Mzee Segua kwa mapenzi yaliyopitiliza mbele ya tabora Jazz, alidiriki kukakataa uhamisho kwenda Wilaya ya Urambo, akitoa sharti ili aende huko basi Bendi hiyo nayo ihamishiwe Urambo. Yaelezwa kwamba baadaye alifukuzwa kazi.


Kikosi kamili cha wanamuziki waliokuwa wakiunda kikosi kamili cha bendi hiyo kilikuwa cha akina  Athumani Tembo kwa upande wa gitaa la Soloakisaidiana na  Shem Ibrahim Karenga aliyekuwa akipiga gitaa la solo, akitunga na kuimba.  Salumu Luzira  alikuwa akiliungurumisha gitaa zito besi na  ugeweza kulilingalinisha na alivyokuwa akipiga Suleiman Mwanyiro ama Lofombo wa  Empire Bakuba.

Wengine katika safu hiyo walikuwa  Kassim Kaluwona, aliyekuwa akilicharaza gitaa la rhythm akisaidiana na  Issa Ramadhani ‘Baba Isaya’  Waimbaji walikuwa ni akina Ramadhani Hamis Nguligwa, Ismail Mwangoko, na Msafiri  Haruob, ambaye baadaye alijiunga na Mwenge Jazz ya Jijini Dar es Salaam.

Kuna msemo wa waswahili usemao kwamba ‘ Vizuri huigwa na Vitamu huonjwa’  Msemo huo ulijidhihirisha wazi kwa Bendi kubwa toka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo ya Soukos Stars, ambayo iliiba nyimbo za Dada Asha wa Tabora Jazz na Vigeregere wa Western Jazz.


Kwa umahiri mkubwa wa bendi hiyo ya  Soukous Stars ilitoka na mseto wa nyimbo nyingi zikiwemo za Dada Asha na Vigeregere  katika album moja ya ‘ Nairobi by Night’

Shem Karenga alijaribu kufuatilia  haki miliki yake pasipo mafanikio kwa kuwa nchi yetu ilikuwa bado haijatunga sheria ya haki miliki.

Tabora Jazz iliposambaratika mwaka 1980, sanjari na Bendi za Nyanyembe Jazz na Kiko Kids, nazo zilienda mrama na baadaye kuondoka katika taswira ya muziki hapa nchini.
Kutoweka kwa Bendi hizo kuliwaacha wapenzi wa muziki wa dansi wa mji huo ambao waliupachika jina la ‘Mboka’ wakijawa na simanzi tele, licha ya kuanzishwa kwa bendi nyingine ya Tabora Jazz ‘Sensema Malunde’ ambayo imeibuka miaka ya karibuni ikiwapa burudani.


Bendi ya Tabora Jazz ilikuwa na makazi yake mjini Tabora ikipiga muziki wake katika ukumbi wa  nyumbani wa Lumumba.
Nyimbo nyingi za bendi hiyo zilipigwa mno kwenye kumbi za starehe pamoja na kituo cha Radio Tanzania Dar es Salaam(RTD) na vituo vingine vya Radio vya Afrika ya mashariki.
Tabora Jazz ilitamba kwa mitindo yake ya za Segere Matata, Segua Segua na  Mambo Mileka.
Mji wa Tabora unaelezwa kwamba ulianza kupata burudani za muziki wa dansi  hata kabla ya chama cha TANU hakichaanzishwa.
Kwa mujibu wa Hassan Athuman ambaye aliyekuwa mwanamuziki wa enzi hizo akipiga gita la solo katika bendi za Tabora Jazz, Kiko Kids, Nyanyembe Jazz  na Milambo Jazz ‘Sona Sona’ kwa nyakati tofauti.
Alisimulia kuwa  mnamo mwaka 1953 ilianzishwa bendi ya muziki wa dansi iliyopewa jina la Staff Jazz ikiongozwa na Hamisi Wampa.
Vyombo vya muziki vya bendi hiyo vilinunuliwa na mfadhili mmoja wa kabila la Kimmanda’ toka nchini Malawi, aliyenunua vyombo hivyo wakati huo akiwa mfanyakazi wa Bomani. 
Staff Jazz ilikuwa na mdhamini akiitwa  mwalimu Hasanari. Waanzilishi wake walikuwa akina Hamisi Ali Songo ‘ngoma kubwa’ , Hamisi Ngege alikuwa  mpiga ngoma ndogo, Dani Kafumu na Nzige   wapulizaji tarumbeta, Akbaru Hasanari Dremsi ‘ngoma kubwa’ Joseph Kayombo ‘bambo’ mwimbaji, Moshi ‘marakasi’,  Saidi ngoma ndogo’ Haji Sungura ‘mlangoni’, Swedi Mandanda 1953/56/58 Hamisi Issa ‘’trarumbeta’ na ryhtm. Hii ilikuwa kati ya miaka ya 1953 hadi 1958.
Wanamuziki wengine walikuwa akina Abdi Fundi upande wa ‘sax’ Athuman Tembo kuimba na ‘solo’ Zakaria Tenda wema(mwimbaji) Sylvester Chifunda ‘mwimbaji’ Juma Athumani ‘drums’ aka Juma Lumango na Mlekwa Suleimani mmoja wa viongozi. Rajabu Risasi upande wa gita la besi.
Staff Jazz ilikuwa ikipiga muziki kwenye ukumbi wa baa ya Rufita ambayo baadaye ukabadilishwa na kuwa Lumumba uliyokuwa katika kona ya barabara za  Rufita na Kapembe, katikati ya mji wa Tabora.
Bendi hiyo kwa sababu ambazo hazikuainishwa, mwaka 1954 ilisambaratika.
Busara na hekima za Hamis Alli Songo zilimfanya aifufue bendi hiyo mwaka 1956 kwa jina lingine la Tabora Jazz.
Yaelezwa kuwa Mlekwa Selemani aliyekuwa shabiki mkubwa wa bendi ya Kiko Kids, akajiunga na Tabora Jazz na kuwa mmoja wa viongozi wa bendi hiyo.
Mwaka 1958 bendi hiyo ilichukuliwa kwenda Kanda ya Ziwa kwa ajili ya kuhamashisha nguvu ya chama cha TANU wakiongozana na viongozi wake  Rashid  Mfaume  Kawawa, Mzee Herman Pacha, mama Mosi Tambwe na mumuwe Abdallah Selemani.
Bendi iliporudi Rashidi Hazuruni mwaka 1959 aliondoka kwenda Dar es Salaam akajiunga na Quban Branch iliyokuwa ikiongozwa na Mzee Mwaipungu.
Kati ya mwaka 1960 na 1961 bendi ilikuwa na wapigaji gita la solo wawili akina Abdi Fundi na Matata. Mwaka uliofuatia Athumani Tembo akaongezeka katika ukung’utaji wa gita hilo.
‘Maisha ni kuhangaika’ usemi huu ulijionesha wakati Rashidi Hazuruni aliporejea tena kupiga muziki na Tabora Jazz mwaka 1963.
Tabora Jazz ilisheheni wanamuziki wengi wakiwemo akina Hamisi Wampa aliyekuwa Kiongozi, Hamisi Alli Songo na Akbaru Hasanari Dremsi walikuwa wadunda ngoma kubwa, Mambosasa alikuwa akipiga ukulele (gita la kizamani). Mambosasa ndiye aliyekuwa baba yake mzazi na Athumani Mambosasa, aliyewahi kuwa mlinda mlango wa Klabu  ya Simba.
Said na Hamis Ngege walikuwa wakipiga  ngoma ndogo, Dani Kafundu na  Nzige walikuwa wapulizaji wa tarumbeta wakati Joseph Kayombo ‘Bambo’ alikuwa mwimbaji.
Kwa upande wa marakasi alikuwemo Moshi, Haji Sungura aliyekuwa mlinzi ‘mlangoni’, Swedi Mandanda alikuwa mcharazaji wa gita la solo, Hamisi Issa alikuwa akipiga gita la kati ‘rhythm’ na Tarumbeta. 
Wanamziki wengine walikuwa Athumani Tembo kwenye solo, upande wa gita la  rhythm walikuwa Hamis Issa na Fundi Hassan Athumani.
Besi liliungurumishwa na Kassim Mponda aliyeondoka katika bendi hiyo mwaka 1965 mwishoni, akifuatana wanamuziki wengine akina Rashidi Hazuruni na Omari Kayanda wakaenda kujiunga na Western Jazz.
Mwaka 1966 Tabora Jazz ikapata mpiga solo mwingine aliyejulikana kwa jina la Stan kuziba pengo la Rashidi Hanzuruni.
Upande wa safu ya waimbaji walikuwa Atrhumani Tembo, Omari Kayanda , Sylvester Chifunda na Joseph Kayombo ‘Bambo’
Mpigaji bongos (ngoma ndogo) alikuwa Juma Athumani ‘kisegeju’ Abdi Fundi alikuwa akipuliza saxophone ’mdomo wa bata’
Kati ya mwaka 1964 na 1965, Tabora Jazz walirekodi nyimbo baadhi yake zikiwa za Ndugu sikilizeni, Tuambie, Dunia haina mwisho, Mwanawanyeje na nyinginezo.
Mwaka 1967 Kassimu Kaluwona  alikwenda Kigoma na kuweza kuwaleta Wema Abdallah, Hamis Kitambi, Issa Ramadhani ‘ ‘Baba Watoto’ Mabrushi
 Ramadhani Mgoligwa na  Hamisi Mkongo.
Mwaka 1968 Salumu Luzira akaijunga na  Tabora Jazz akitokea Nzega.
Mwaka 1971 Wema Abdallah akaondoka Tabora Jazz akaenda Western Jazz, nafasi yake ikachukuliwa na mpiga solo mwingine aliyejulikana ka jina la Kalii, alikitokea Kigoma Jazz.
Kwa kipindi kifupi Said Mabera na Hassan Rehan Bichuka nao walijiunga na Tabora Jazz wakitokea Rumonge Jazz.
Shem Karenga aliletwa na Kassim Kaluwona toka Kigoma, kuja Tabora kujiunga na bendi hiyo Aprili 1972.
Shem baada ya kutua, alishiriki vilivyo katika utengenezaji wa wimbo wa Dada Asha ambao baadaye
Wimbo wa Dada Asha uliibwa na bendi ya Sokous Stars ya akina Lokassa ya Mbongo ya nchini Kongo na kuichakachua  ukiwemo wimbo wa Vigeregere uliopigwa na Western Jazz. Pia mwanamuziki Lita Bembo na vijana wake wa  Stukas nao walikwapua na kuupiga wimbo huo.
Kwa mujibu wa Hassan Athumani amsema kuwa wimbo wa Dada Asha, mtunzi wake alikuwa askari jeshi aliyeomba atengenezewe wimbo huo.
Tabu Ley aliiona album yenye wimbo huo wa Dada Asha akiwa Nairobi na aliinunua akaenda kuiuza nchini Kongo, Poland na Ubelgiji.
Bendi hiyo baadaye akajipanga upya kwa kupata damu changa ili kuendeleza muziki wake.
Iliongeza watunzi na waimbaji wengi akiwemo Msafiri Horoub,  Madaraka Morris, Ismail Wangoko na wengine wengi.
Kwa umoja wao wakafyatua nyimbo nyingi zilizoweza kuridhisha nyoyo za wapenzi na mashabiki wa Tabora Jazz. Nyimbo hizo ni Ashura, Helena, Mapenzi ulimi, Visa uache, Lucie umeniacha, Zabibun na Niambie leo Kaka. Ziningine zilikuwa za Usijifanye Mwewe, Mariam mpenzi, Zabibu No.2, Sofia mpenzi,  Tatu, Serafina, Tamaa yako na  Asha No. 1. Zote hizo  zilikuwa zikitamba mno wakati huo. Zingine ni pamoja na Alhamdulilah, Nashukuru sana, na Dada Asha.
Nyingine ni pamoja na Dada Mwantumu, Ujana una mwisho, mwisho wake ni uzee. Zingine zilikuwa za Salima, Mapenzi Ulimi, Dada Remmy na Rukia wajidanganya.
Wanamuziki wengi wanatajwa katika bendi hii ya Tabora Jazz, baadhi yao wapo hai kama vile Shem Karenga, Ramadhani Mwanangwa (rhythm) Salumu Luzira na wengine wengi.
Baadhi ya wanamuziki wanaotajwa katika makala hii wamekwishafariki.
Walio haihaajishughulishi tena na maswala ya muziki kufuatia umri kuwatupa mkono.
Bendi ya Tabora Jazz haipo tena katika ulimwengu wa muziki.
Mwisho.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni