Alhamisi, 21 Desemba 2017

Kambi walimoshambuliwa walinda amani wa Tanzania huko DRC yaimarishwa




Umoja wa Mataifa umesema kambi ya Semuliki huko Kivu Kaskazini nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC ambayo ilishambuliwa tarehe 7 mwezi huu na kusababisha vifo vya walinda amani 14 wa Tanzania na wengine 44 kujeruhiwa sasa inaimarishwa.
Mkuu wa operesheni za ulinzi wa amani kwenye Umoja wa Mataifa Jean-Pierre Lacroix amesema hayo baada ya kuzuru eneo hilo na kuona jinsi kambi hiyo ikijengwa kwa uthabiti zaidi na ulinzi kuimarishwa wakati huu uchunguzi wa tukio hilo ukisubiriwa kwa hamu.
Akihojiwa na Radio Okapi ya ujumbe wa Umoja wa Mataifa huko DRC, MONUSCO, Bwana Lacroix amezungumzia pia uchunguzi wa tukio hilo..

  Uchunguzi utafanyika kwa  mbinu ambazo zinatakiwa. Hitimisho na mapendekezo  yake yatachambuliwa kwa kina na kuzingatiwa kwa hali ya juu na kwa haraka iwezekanavyo. »


Alipoulizwa kuhusu ujumbe wake kwa raia wa DRC wakati huu wa kuelekea mwaka mpya, Bwana Lacroix amesema..

 Kwa wananchi wa DRC, nawaeleza kuwa MONUSCO na Umoja wa Mataifa tuko pamoja nao. Kuna nyakati kunakuwa na vikwazo ambapo hatutekelezi majukumu kama ipasavyo. Lakini tuafanya kwa kadri ya  uwezo wetu na kufanya kazi kila siku ili kunufaisha raia wa DRC. »

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni